Naibu Waziri wa wizara hiyo, Damas Ndumbaro, alieleza hayo wakati akijibu swali la msingi lililoulizwa na Mbunge wa Gando (CUF), Othuman Omari Haji, aliyetaka kujua mpango wa serikali wa kuandaa sera mpya ya mambo ya nje umefikia hatua gani.
Dkt Ndumbaro: "Wizara yake imekamilisha uandaaji wa Rasimu ya Sera ya Mambo ya Nje kama ilivyopendekezwa na wadau wakati wa kufanya tathmini ya utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje ya mwaka 2001."
Vyanzo vya habari vimeripoti kuwa rasimu hiyo iko katika hatua ya kusambazwa kwa wadau mbalimbali kama vile wizara, idara na taasisi za serikali, sekta binafsi na Taasisi zisizo za kiserikali, ili kupata maoni yanayolenga kuboresha zaidi.
Rasimu hiyo ina maeneo mapya ambayo yamejumuishwa katika sera iliyopendekezwa ni pamoja na kutambua na kuwajumuisha diaspora kwenye juhudi za kuleta maendeleo ya taifa, kutambua mihimili mingine kama wadau wa sera (Bunge na Mahakama) na kuzingatia mikakati na mipango ya muda mrefu ya nchi na Jumuiya za Kikanda na Kimataifa.
Ripoti hiyo inaeleza kuwa utekelezaji wa sera hiyo itafika hadi ngazi ya wilaya na mikoa, vijana na tasnia ya michezo na burudani kutumika kama njia ya kuitangaza Tanzania nje.
Jengine ni kuwa rasimu ya sera inaelekeza nchi kuimarisha uhusiano na nchi nyingine yanayolenga kukuza uchumi wa nchi kwa kuzingatia mipango ya muda mfupi na mirefu ya serikali.