Mahakama Kenya yatoa hukumu kamili ya kubatilishwa uchaguzi

Jaji mkuu wa Kenya David Maraga (Kulia0 na naibu wake, Philemona Mwilu.

Mahakama ya Juu nchini Kenya, Jumatano imetoa hukumu kamili juu ya uamuzi wa kesi iliyowasilishwa na mgombea uchaguzi wa muungano wa National Super Alliance (Nasa).

Katika zoezi hilo la kutoa hukumu kamili juu ya kubatilishwa uchaguzi wa urais jopo la majaji watano lilikuwa mahakamani likiongozwa na Jaji Mkuu, David Maraga.

Katika maelezo hayo kamili, Jaji Maraga, naibu wake Philomena Mwilu, Majaji Isaac Lenaola na Smoking Wanjala, walishikilia kwamba licha ya kukosolewa kwa uamuzi wao na baadhi ya Wakenya, kulikuwa na haja ya kubatilisha uchaguzi huo wa urais wa tarehe 8 mwezi Agosti.

Hatua hiyo ilifuatia uamuzi mfupi uliotolewa tarehe mosi mwezi Septemba ambao ulibatilisha uchaguzi wa rais Uhuru Kenyatta kama rais, kufuatia tangazo la tume ya uchaguzi, IEBC, kwamba alikuwa ameshinda kwenye kinyang'anyiro hicho.

Akisoma uaumuzi huo, jaji Isaac Lenaola alianza kwa kueleza maombi yaliyokuwa yametolewa na Bw Odinga kupitia mawakili wake na pia jinsi upande wa utetezi ulivyojibu.

Jaji Mwilu alisema kulikuwa na dosari nyingi kwenye zoezi hilo, na kuongeza kuwa tume ya IEBC ilikiuka amri ya mahakama iliyoitaka kuwaruhusu mawakala wa pande zote mbili kukagua sava za mfumo wake na kupata habari zilizohitajika.

"Maoni yetu ni kwamba walikataa kutimiza amri ya mahakama," alisema jaji huyo.

Majaji Jackton Ojwang na Njoki Ndung'u pia walisoma uamuzi wao ambao ulitofautiana na ule wa majaji wenzao wanne.

Hata ingawa jaji Wanjala hakuwa mahakani, jaji mkuu Maraga alisema kuwa alikuwa ametia saini uamuzi huo na kwamba ailikuwa amesafiri nje ya nchi.

Tayari tume ya IEBC imetangaza tarehe ya uchaguzi wa marudio kuwa Oktoba 17 huku muungano wa Nasa ukitoa vikwazo kadhaa kabla ya kukubali kushiriki uchaguzi huo.

Habari zaidi itafuata...