Kituo cha televisheni cha Al Arabiya kimeonyesha picha za moshi mzito ukitoka kwenye jengo moja katika mji mkuu kutokana na mfululizo wa milipuko ya mabomu yenye sauti kubwa.
Eneo la makazi ya watu likifuka moshi kutokana na mashambulizi yanayoendelea katika mapigano ya majenerali wawili upande wa mashariki ya Khartoum. (Photo by AFP)
Kuzuka ghafla kwa mapigano mwishoni mwa wiki baina ya majenerali wawili wa juu wote wanaungwa mkono na maelfu ya wapiganaji wenye silaha nzito, hali hiyo imewasababisha watu kukwama katika nyumba zao au mahali popote wanapoweza kupata hifadhi.
Bidhaa muhimu zimeanza kupungua na hospitali kadhaa zimelazimika kufungwa. Wakati huo huo msemaji wa vikosi vya Sudan alisema Jumanne jeshi lilikuwa limeshika udhibiti wa shirika la utangazi la serikali.
Mgonjwa akiwasili hospitali mjini Khartoum, Sudan, Jumatatu, Aprili 17, 2023. Hospitali katika mji mkuu zimeelemewa wakati jiji hilo likigeuka kuwa ni ukanda wa vita katika mapigano ya vikosi vya majenerali wawili. Takriban hospitali sita kati ya 20 Khartoum na mji wa jirani wa Omdurman zimefungwa, umoja wa madaktari unaeleza. (AP Photo/Ashraf Idriss)
Televisheni ya Sudan inayoendeshwa na serikali ilirusha mazungumzo ya simu na Brigedia Jenerali Nabil Abdullah ambapo alidai hali ilikuwa imedhibitiwa kabisa.
Aliongeza kusema kuwa jeshi la Sudan halitaki kupanua operesheni zake katika hatua iliyopo sasa. Jeshi na kikosi cha RSF walikuwa wanapigana pia katika miji mikubwa katikati kuzunguuka nchi hiyo ikiwemo magharibi mwa Darfur na sehemu ya kaskazini na mashariki zinazopakana na Misri na Ethiopia.
Mapigano ni sehemu ya kugombea madaraka kati ya Jenerali Abdel Fattah Burhan mkuu wa vikosi vya jeshi, na Jenerali Mohamed Hamdan Dagalo mkuu wa RSF.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken amesema Jumanne kwamba mwanadiplomasia wa juu wa Marekani alishambuliwa huko Sudan na amesisitiza umuhimu wa kusitisha mapigano.
Blinken alizungumza katika mji wa kifahari wa Karuizawa huko Japan muda mfupi baada ya kufunga mazungumzo ya kundi la G7.